Maskini!! MWANAMKE HUYU AMWAGIWA MAFUTA YA MOTO KISHA KUCHUNWA NGOZI...CHANZO MGOGORO WA KUSAFISHA CHOO

Rehema Gwaya akiwa na majeraha usoni baada ya kumwagiwa mafuta ya moto


“Dunia imeharibika na binadamu hawana upendo wamegeuka kuwa na tabia kama za wanyama kila kukicha…” hiyo ni kauli yake Rehema Gwaya (41) mkazi wa Barabara ya Sokoine, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.

Rehema ambaye ni mjasiriamali mdogo anayejishughulisha na kuuza juisi, alipatwa na mkasa wa kumwagiwa mafuta ya moto ya kupikia ambayo yalikuwa yanatumika kwa ajili ya kuchomea maandazi.


Inadaiwa aliyefanya unyama huo ni mke wa shemeji yake baada ya kutokea sintofahamu ya usafi wa mazingira ya nyumbani kwao, kama anavyojieleza:


“Tukio limetokea mwishoni mwa Mei nikalazwa mwanzoni mwa Juni hadi sasa Julai ambapo Daima Said (13) ambaye ni mwanafunzi wa Shule ya Msingi Luseti ninayeishi naye aligombana na mke wa shemeji yangu, Zefania Chimgege, chanzo kikiwa ni suala la usafi wa mazingira kwani mama huyo alipaswa kwenda kusafisha choo akakataa kukawa na mzozo mkubwa.


“Mzozo huo ulitokea mimi nikiwa sipo, nilikuwa kwenye biashara zangu, niliporudi nyumbani nilimfuata mama Chimgege ili anipe maelezo, ghafla akanivamia na kuanza kunishambulia kwa maneno makali yaliyoambatana na matusi.


“Wakati huo mume wake alikuwa anachoma maandazi kwa ajili ya biashara yake, wakati naendelea kutafakari kauli chafu alizozitoa dhidi yangu, nilishitukia nikimwagiwa mafuta ya moto usoni, papo hapo nilianguka chini jambo lililompa nafasi mama huyo kunikalia na kuanza kunichuna ngozi iliyobabuka.


“Nilipoteza fahamu na kujikuta nipo Hospitali ya Mkoa Songea, nimelazwa wodi ya wanawake nikiwa na majeruhi usoni na kwenye matiti, hivyo naendelea kupata matibabu.


“Nawaomba Watanzania wenye mapenzi mema kunisaidia kwani kwa sasa siwezi kufanya shughuli yoyote kutokana na kuuguza majeraha ya moto ambayo yana maumivu makali na hapa nilipo nina mtoto mdogo wa miezi tisa ambaye ananyonya.


Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Serikali ya Mkoa Songea, Dk. Benedikto Ngaiza amethibitisha kumpokea mgonjwa huyo ambapo alisema anaendelea kupatiwa matibabu.


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, ACP Mihayo Mikhela amekiri kutokea kwa tukio hilo na amethibitisha kuwa mtuhumiwa anashikiliwa wakati upelelezi unaendelea.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527