MGEJA "HAKUNA MGOMBEA WA CCM ATAKAYEKATWA JINA LAKE"



Kufuatia hofu iliyotanda ya baadhi ya wagombea  kukatwa majaina yao Chama Cha mapinduzi Mkoani Shinyanga kimewatoa hofu wanachama wake kwamba hakutakuwa na utaratibu wa kuwakata baadhi ya  majina  wagombea wa ngazi ya udiwani na wabunge katika kipindi cha uchaguzi mkuu ujao utakao fanyika mwezi Oktoba 2015.


Kauli hiyo imetolewa juzi na mwenyekiti wa CCM mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja wakati akizungumza kwenye sherehe za ushindi wa serikali za mitaa 2014  zilizofanyika katika kijiji cha Nyandekwa kata ya Nyandekwa wilayani Kahama na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa chama wilaya na mkoa.

Mgeja alisema CCM mkoa wa Shinyanga haina agenda ya kukata jina la mgombea atakayekubalika kwa wananchi na kwamba  maneno yanayozushwa na baadhi ya wanachama mbalimbali yana lengo la kupotosha wanachama na wananchi.

“Haya maneno yanayozushwa yana lengo la kuwakatisha tamaa baadhi ya wanachama wenye nia ya kugombea nyadhifa mbalimbali katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwaka huu 2015,naombeni muwapuuze”,alisema Mgeja.

Mgeja alisema CCM itatenda haki kwa kila mwanachama  atakayegombea nafasi yeyote ndani ya chama na kuongeza kuwa suala la mwanachama la kuchaguliwa ama kutochaguliwa ni suala la wanachama ndiyo watakaoamua kupitia mikutano halali ya chama.


Aidha aliwatahadharisha viongozi wa CCM mkoani Shinyanga humo wasiwachagulie wagombea wanachama na wananchi kwani kufanya hivyo ni sawa na kutengeneza bomu ambalo linaweza kulipuka Oktoba 2015 na hakuna mtu au kiongozi yeyote ndani ya chama atayeweza kulizima.

Katika hatua nyingine Mgeja alitoa onyo kali kwa baadhi ya wanachama wenye nia ya kugombea  ambao wameanza kupita pita kwenye majimbo na kata kwa kutumia jina la “Ikulu” kuwa wametumwa na Ikulu kwa lengo la kuungwa mkono hali ambayo aliikemea vikali na kuagiza viongozi ngazi za Wilaya na kata kufuatilia nyendo zao na kuwataka kuacha  tabia hiyo mara moja.


Aidha alitoa angalizo kwa wagombea wenye nia ya kusubiria kubebwa au kupakatwa na wakubwa kwani kwa uchaguzi wa sasa hauna nafasi kwa watu kama hao bali watu hao watajiuza wenyewe ndani na nje ya chama kwa historia ya utendaji wao wa kazi ambao ndiyo utakaowabeba.


“Nitoe angalizo kwa wale wote wenye nia ya kusubiri kubebwa na ama kupakatwa na wakubwa niwambie tu uchaguzi huu wa sasa hauna nafasi kwa watu kama hao bali watajitangaza na kujiuza wenyewe kwa historia ya utendaji wao wakazi ambao ndiyo utakao wabeba”,aliongeza Mgeja.

Hata hivyo Mgeja aliwapongeza viongozi na wanaCCM  wa kata ya Nyandekwa wilayani Kahama kwa ushindi wa asilimia mia moja katika uchaguzi wa serikali za mitaa na kuongeza kuwa ushindi huo wa kishindo umetokana na viongozi kuteua wagombea wazuri waliokubalika kwa wananchi.


Kata hiyo ya Nyandekwa yenye vijiji saba ambavyo ni Nyandekwa,Chalya,Lowa,Kakebe,Kalengwe,Kigungumuli na Baduha ambapo katika uchaguzi wa serikali za mitaa Chama Cha Mapinduzi kilishinda viti vyote kwa asilimia 100  na hivyo kupelekea kata hiyo kuandaa sherehe za ushindi ambapo mgeni rasmi katika sherehe hiyo alikuwa ni mwenyekiti wa CCM mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja.
Na Kadama Malunde-Kahama

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527